Lesson Text/Footnote View
Read this if you can't see the following text in the correct font


Mzee Kulwa ni mkulima maarufu sana katika kijiji cha Gagagege. Yeye na familia yake pia ni wafugaji. Kijiji cha Mzee Kulwa kiko kandokando mwa ziwa, hivyo mzee huyu pamoja na jirani zake wanavua samaki pia, hasa wakati wa masika.

Mzee Kulwa hivi sasa ana umri wa kama miaka tisini. Tunakisia umri wake kwani anakumbuka kwamba alipokuwa mwenye umri wa "kuchunga ng'ombe", Waingereza walianza kutawala Tanzania. Ingawaje uzee umepunguza nguvu za Bwana Kulwa, bado anaweza kufanya kazi shambani na hupenda sana kwenda ziwani na wajukuu zake na huwafundisha Kigagagege.

Wagagagege ni watu wataratibu sana na bado wanafuata mila zao za zamani. Mzee Kulwa ni kiongozi wa shirika la wazee. Wazee wa kijiji hiki wanaheshimiwa sana na wanakijiji. Wazee hawa bado wana sauti kubwa katika mipango ya maendeleo ya kijiji, na wanajadili na kuhukumu kesi ndogondogo za wanakijiji. Ingawaje Mzee Kulwa amekubali mabadiliko na maendeleo ya kijiji chake, bado anasisitiza sana vijana watunze na kuheshimu mila na desturi za kabila lake. Hata leo, Mzee Kulwa hasiti kumsema na hata kumuadhibu yeyote kijijini!

Tumtakie Mzee Kulwa na Wazee wengine kama yeye maisha mema na yenye furaha.

Copyright (c) 2001 Arizona Board of Regents
Created with MaxAuthor(tm)